Sunday 20 May 2012

Wakati umewadia

Uwanjani najitoma, jameni nipokeeni
Ni mengi lonisukuma, nafasi kuwaombeni
Vijana tunalalama, sie tuko mashakani
Wakati umewadia, vijana tugutukeni
 
Viongozi chipukizi, watuita mahasidi
Tufanyeni uamuzi, katu tusikaidi
Waache hao wapuzi, walojaa ufisadi
Wakati umewadia, vijana tugutukeni
 
Huu ni wakati wetu, vijana kujitokeza
Piganie haki zetu, tuwaonyeshe twaweza
Tulinde ujana wetu, mie ninawahimiza
Wakati umewadia, vijana tugutukeni
 
Taratibu taratibu, tutafika kileleni
Nauliza mnijibu, kesho itafika lini?
Tuwang'atue mababu, walio mamlakani
Wakati umewadia, vijana tugutukeni
 
Tamatino nimefika, lilobaki ni vitendo
Twafaa kujumuika, kimawazo na mwenendo
Rabuka tupe baraka, tujalie na upendo
Wakati umewadia, vijana tugutukeni